mPIGA KURA

Jumapili ya Tarehe 25 Oktoba, mamilioni ya Watanzania watapiga kura kuchagua viongozi watakaowaongoza kwa miaka mitano ijayo. Huu utakuwa uchaguzi wa sita toka nchi hiyo iliporejea kwenye siasa ya mfumo wa vyama vingi mwaka 1992.

Kama ilivyo kwa chaguzi zote duniani kuna mambo ya msingi ambayo hutoa taswira ya mchakato mzima utakavyokuwa, na kwa upande wa Tanzania kuna mambo matano ambayo ni ya muhimu kuyafahamu.

Short presentational grey line

Magufuli vs Lissu ama Magufuli vs Membe?

Toka uchaguzi wa kwanza wa mwaka 1995, mbio za uchaguzi nchini Tanzania huongozwa na vinara wa kinyang'anyiro cha urais.

Mvuto na ushawishi wa wagombea wa chama tawala cha CCM na upinzani huwa ndiyo jambo linalotawala zaidi katika vinywa vya wapiga kura zaidi ya sera na ilani zao.

Mwaka 1995, kinyang'anyiro kilikuwa baina ya Benjamin Mkapa wa CCM na Augustino Mrema wa NCCR-Mageuzi, na licha ya kupokea upinzani mkali Mkapa aliibuka na ushindi kwa 61% ya kura. Mwaka 2000, Mkapa aligombea muhula wa pili na kwa wakati huo mpinzani mkuu alikuwa Prof Ibrahim Lipumba wa CUF. Hata hivyo nguvu ya upinzani iliporomoka na Mkapa akaibuka na ushindi wa 71%.

Uchaguzi wa mwaka 2005 CCM ilimsimamisha Jakaya Kikwete ambaye alikuwa na ushawishi mkubwa na kuzoa 80% ya kura, Prof Lipumba alimfuatia kwa mbali akipata 10% ya kura. Mwaka 2010 Kikwete aligombea kwa muhula wa pili dhidi ya Dkt Wilboad Slaa wa Chadema. Ushawishi wa upinzani ulipanda, japo Kikwete alirudi madarakani lakini alishinda kwa 62% ya kura.

Miaka mitano iliyopita CCM ilimsimamisha John Magufuli, huku upinzani ukimsimamisha Edward Lowassa. Ulikuwa mchuano mkali kweli kweli na kwa mara ya kwanza toka siasa za vyama vingi kurejea Tanzania, mgombea wa CCM hakufikisha 60% ya kura. Magufuli alipata 58% ya kura huku Lowassa akipata 39%.

Tundu Lissu ametangaza nia ya kuchuana na Magufuli Oktoba
Maelezo ya picha,

Tundu Lissu ametangaza nia ya kuchuana na Magufuli Oktoba

Mwaka huu 2020, Magufuli ndiye mgombea pekee aliyechukua fomu ya kugombea urais kupitia CCM, hivyo ni dhahiri kuwa atapambana kurejea kwa muhula wa pili na wa mwisho madarakani kwa mujibu wa katiba. Kete yake kubwa katika uchaguzi ujao utakuwa rekodi yake ya kuleta mabadiliko na maendeleo ya kasi katika sekta muhimu za uchumi kama, ujenzi, uchukuzi na afya.

Kwa upande wa upinzani mpaka sasa, bado haijakuwa wazi ni nani atakuwa kinara wao. Kwa upande wa chama kikuu cha upinzani Chadema, aliyekuwa mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu anaongoza mbio za kupewa ridhaa na chama chake. Lissu amekuwa ni moja ya wakosoaji wakubwa wa serikali ya Magufuli, mwaka 2017 alishambuliwa vibaya kwa risasi, na kulazimika kupelekwa ughaibuni kwa matibabu.

Mpaka sasa bado yungali ughaibuni, na hata fomu ya kugombea urais ndani ya chama amechukuliwa na mwakilishi. Mara kadhaa amekuwa akiahirisha kurejea Tanzania akitaja sababu za kiusalama. Kwa sasa ameahidi kurejea Julai 28. Nguvu ya Lissu ipo katika ujenzi wake wa hoja, na uwezo wake wa kumkabili Magufuli.

Mwanansiasa mwengine ambaye anatarajiwa kugombea kwa tiketi ya upinzani ni Bernard Membe. Membe amehudumu kama Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania wakati wa Kikwete na alikuwa ni moja ya mawaziri wenye nguvu na ushawishi mkubwa. Hata hivyo, toka alipoingia madarakani Magufuli, alikuwa akitajwa kuwa anamhujumu kwa kupanga kuchuana naye ndani ya chama mwaka huu. Mwanasiasa huyo alifukuzwa uanachama wa CCM na wiki hii amerejesha kadi ya uanachama.

Japo bado hajajiunga rasmi na upinzani, duru za kisisasa zinaonesha kuwa kuna harakati zinaendelea baina yake na chama cha ACT-Wazalendo. Wiki ilopita, Membe aliiambia BBC kuwa atagombea urais endapo upinzani utaungana na kumuomba agombee kwa mwamvuli wao.